Monday, March 21, 2016

JINSI YA KUPATA WAZO LITAKALO KUPATIA PESA



Habari za leo ndugu zangu,
Leo napenda nizungumzie jambo moja muhimu sana katika maisha yetu.
Jambo hilo ni “WAZO”  kwa Kiingereza wanaita ‘Idea’.  Kama nilivyo wahi kusema kila mtu ukimuuliza kwa nini hajafanikiwa kwa kiwango anachotakiwa atakuambia kuwa tatizo ni ‘PESA’  hana kabisa au hazitoshi!
Lakini kwa kweli mara nyingi kama sio mara zote, tatizo huwa siyo ukosefu wa pesa bali huwa ni ukosefu wa “WAZO” sahihi litakalo kupa pesa.
Hivyo leo nataka tuone jinsi ya kupata wazo ambalo litaweza kukupa pesa.
Kabla sijakupa mbinu za kupata wazo ambalo laweza kukupa pesa na siyo pesa tu, bali hata utajiri ngoja nikupitishe mahali fulani ili uweze kufungua macho yako vizuri zaidi kupitia maswali haya:
Je, unajua kuwa dawa ya meno unayotumia ni wazo la mtu? Kuna mtu aliwaza kuwa watu wanahitaji kusafisha vinywa vyao hivyo akapata wazo la kutengeneza dawa ya meno.
Je, unajua kuwa Amerika iligunduliwa na mtu ambaye alikuwa na wazo kuwa kama akisafiri kuelekea magharibi atafika kwenye nchi ambayo hakuna baharia aliyewahi kuifikia? Christopher Columbus alikuwa mtu huyo na kupitia wazo lake hilo alifika Amerika siku moja, nchi mpya. Kwa nini alikuwa na wazo la kufika nchi mpya na pia kutafuta njia fupi ya kuifikia India lakini akafika Amerika na ukawa ugunduzi wa kihistoria kutoka na “wazo”!
Ili uweze kupata wazo zuri litakalo kupatia pesa jifunze kufanya yafuatayo:-
1.       Jifunze kuona kupitia akili yako na siyo macho yako.
 Namaanisha unapokuwa unatembea unaposikia watu wakilalamikia kuhusu hali fulani, au unaweza kuona jambo fulani ambalo haliko sawa basi anza kujiuliza kwa nini hali iko hivyo. Kupitia kujiuliza kwako tayari utashangaa unapata WAZO la kukabiliana na tatizo husika ambapo wengi huita “FURSA”

2.       Andika juu ya wazo lolote zuri linalokujia kwenye ubongo wako
Watu wengi huwa wanapata mawazo mazuri ambayo yangeweza kubadilisha maisha ya mamilioni ya watu wakaishi kwenye hali bora zaidi, lakini kwa kuwa hawajajizoeza kuweka kumbukumbu muda mfupi tu mawazo hayo hupotea.

3.       Soma vitabu
Jambo jingine linaloweza kukusaidia kupata wazo ambalo laweza kukufanya kuwa milionea ni kusoma vitabu. Hapa simaanishi usome vitabu vya tamthilia, HAPANA namaanisha vitabu vya maarifa mbalimbali. Kwa mfano ukitaka kujua Barak Obama rais wa sasa wa Amerika (Barak Obama alikuwa madarakani 2008-2016) nenda kasome vitabu vyake na hasa hii inawafaa wale watu wanaotaka kuwa wanasiasa mahiri.
Ukitaka kujua jinsi Warren Buffet alivyo faulu kuwa tajiri mkubwa huko Amerika soma habari zake. Ninacho jaribu kukuambia hapa ni kwamba kupitia kusoma vitabu vya watu mbalimbali utashangaa unaanza kupata wazo lako la namna ya kutoka kimaisha.

4.       Safiri
Kusafiri ni mbinu nyingine ya kupata wazo la kukutoa kimaisha. Watanzania wengi hatupendi au hatuna kawaida ya kusafiri. Mtu akisafiri ni kwa sababu kuna shida fulani imemsukuma kufanya hivyo!
Jambo hili siyo sahihi kabisa, hebu jizoeze kusafiri kwa lengo la kujifunza na kupitia safari hizi utashangaa utapata wazo la biashara ambalo litakutoa kimaisha.

5.       Anzisha mjadala wenye lengo maalum
Njia nyingine ya kupata wazo ni kuanzisha mjadala kwa lengo la kupata wazo jipya. Mbinu hii unapaswa uitumie kwa watu ambao wamekuzoea kwa mfano wanamichezo wenzako, marafiki zako, wafanyakazi wenzako na kadhalika.
Unaweza kuanza kwa kuuliza maswali yafuatayo (huu ni mfano tu)
Je, miaka mitano au kumi ijayo huu mji wetu utakuwa na tatizo gani kubwa?
Je, ni nini kinaweza kufanyika ili kuweza kukabiliana na hali hiyo wakati huo? (WAZO)
Utashangaa kwa njia hizi nilizo eleza hapo juu unaweza kuja na wazo zuri sana la kukutoa kimaisha.

Kuanzia sasa usikae tu, anza kuchukua hatua.
·         Uwe na tabia ya kutembea na kalamu na karatasi na uandike kila wazo zuri linalokujia na jaribu kufanya utafiti juu ya namna ya kulitekeleza
·         Uwe na tabia ya kujisomea, jifunze juu ya watu waliofanikiwa jinsi walivyo fikia hatua hiyo
·         Nenda kaongee na mtu aliyefanikiwa muulize mbinu alizopitia hadi kufikia mafanikio yake
·         Uwe mvumilivu katika kutekeleza wazo lako kumbuka Roma haikujengwa kwa siku moja
Mwisho niseme tu kuwa njia za kupata wazo zuri ziko nyingi hizo nilizo zitaja ni baadhi tu.
Kumbuka kuwa wenye fedha yakiwepo na mabenki hawatoi pesa kwa ajili ya kuanzisha biashara mpya.
Lakini hutoa pesa kwa ajili ya kutekeleza wazo bora la Biashara mfano mzuri ni wa Ndugu Regnald Mengi. Amekuwa akitoa pesa kwa ajili ya kusaidia vijana wenye mawazo kama hayo. Siyo hilo tu hata
Shirika la Utangazaji la Uingereza BBC miaka ya hivi karibuni wamekuwa wakiwezesha mawazo mapya ya ubunifu .
ACHA KUWAZA UTAPATA WAPI PESA WAZA NAPATAJE WAZO ZURI LA KUTATUA TATIZO LA JAMII.
Ukipata wazo zuri zaidi umepata kitu cha thamani sana hata kuliko mgodi wa dhahabu kama unadhani nakutania nenda kawaulize wafuatao:
Wamiliki wa kampuni ya Coca Cola, Mmiliki wa Facebook, Mmiliki wa Microsoft, Mmiliki wa Mohamed Enterprises, Mmiliki wa IPP Media na wengine. Pesa iko kwenye utatuzi wa matatizo ya watu na matatizo ya watu hutatuliwa kwa wazo moja tu la ubunifu.
Kazi ni kwako na kwangu kutafuta “WAZO”
Asanteni. 

No comments:

Post a Comment